WE BINTI MREMBO UMEJIANDAAJE NA NDOA, AU UNAKURUPUKA TU?SOMA HILI SOMO


Aih! Jamani hebu tusijitoe akili huu ni mwezi wa toba mwezi wa wastaarabu tuwaache watu wafunge siyo kujipitisha na nguo za matamanio kuwafungulisha wenzenu mchana.Tunaendelea na kiporo chetu naona ushakunja mdomo kwa vile nimekugusa. Dada wewee chuki nichukie lakini yangu yachukue. Sasa tuendelee niliishia wapi vile oo nimekumbuka.


Wanawake wenzangu, kaeni mjue kwamba wanaume wana maudhi ambayo tunatakiwa tuyavumilie, inatupasa wanawake tuwe na moyo wa chuma kuweza kuhimili tabia za wanaume.

Siye tuliyofunzwa zamani katika mkole na msondo tuliambiwa kuwa wanaume wana maudhi  kushinda neno lenyewe maudhi, wana makusudi  kuliko makusudi yenyewe, tena ni kama watoto wadogo wanaotaka kulelewa na hawataki kuelewa wana ujeuri wa kutaka kuabudiwa.

Nani asiyejua, jeuri ya wanaume? Jamani si kila siku tunaambiwa kuhusu unyanyasaji wao katika familia?  
Mateso na manyanyaso yao yote wanawake tunatakiwa tuyavumilie wala tusilie kwani kwa vyovyote vile siye ndiyo liwazo lao la moyo.

Hakuna mwanaume anayeweza kusimama peke yake bila ya mchango wetu! Halo haloooo wanawake tunayo hatunayooo? Jamani usivimbishe mashavu itikia basi... tunayooo!
Kama tunafanya kicheni pati kwa ajili ya kukusanya vyombo, basi tusiache kufuata zile mila na desturi zetu za ndani yaani kufundwa na makungwi na manyakanga wa enzi zile ili tupige ndege wawili kwa jiwe moja.
Tuache kuiga mambo ya kihuni ndani ya ndoa, kwani kwetu siye ndoa ni heshima, tunatakiwa tuilinde na tufuate masharti yake ili tuweze kuheshimika kama mama na bibi zetu walivyoweza kula chumvi nyingi kwenye maisha ya ndoa.

Vitabu vya dini vinasema kwamba, mwanamke mpumbavu ataivunja ndoa yake kwa mikono yake mwenyewe.
Mpo au mmelala? Haya mmelalia nini mikono au masikio? Kikubwa wanawake wenzangu tujifunze kwa waliotutangulia, ndoa zao zilidumu kutokana na kuwaheshimu waume zao.

Hebu waulize waliotangulia kuingia kwenye ndoa kilichowakimbiza ni nini, lazima kwanza watajutia makosa yao kisha  watakwambia kwamba siku zote nazi haishindani na jiwe.Asikuambie mtu ndoa inataka kufuata mafunzo siyo mwanamke kubinua midomo kwani ikikushinda utalia kila uchao na utaongeza idadi ya wanaume na kila atakayekuoa atakuacha kwa kuwa utakuwa umeshindikana.
Wanawake tusiwe kama kuku wa mayai waliozeeka ambao hawafai kwa nyama kwa kukosa ladha, hebu tujiheshimu kwa mavazi na tuifuate elimu hii ili tuzilinde ndoa zetu.

Mwari wangu usije kusema kuwa sijakwambia kwani nimeshasema sana, angalia usichelewe kwani ukichelewa kuuanika utakuja kuutwanga mbichi, badilika bado hujachelewa.

Ni Mimi Anti Nasra Shangingi Mstaafu.



x

;

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »